SHAIRI : SITAFUNGA RAMADHANI!.
Shairi : Sitafunga Ramadhani
Mtunzi : Dully wa mashairi
Tell.......: +255762541601
••••••••••••••••••••••••••••••••••••••••
Ameshafika mgeni nashindwa kumpokea,
haliyangu taabani utazani najifia,
sitafunga Ramadhani mwenzenu ninaugua,
sivunji nguzo ya dini, Mwenyezi ndo anajua.
Yapata mwezi wa pili nasumbuliwa na homa,
Chakula chote me sili nikijaribu chagoma,
Usiku kucha silali nalia na kulalama,
Sijapata afadhali roho yote yaniuma.
Kufunga ninatamani lakini sasa siwezi,
Rafiki niombeeni aninusuru mwenyezi,
Vidonda hadi tumboni ni zaidi ya miezi,
Nahisi kifo kooni yananitisha maradhi.
Kufunga nguzo ya dini ndugu usipuuzie,
Kamilisha Ramadhani thawabu ujipatie,
Kufunga ninatamani yameshanisibu mie,
Nazidi mwomba Manani uhai anijalie.
Nakuomba Mungu wangu kwahili unihifadhi,
Wanijua haliyangu yakwamba nina maradhi,
Watazua walimwengu naigiza sikuhizi,
Naumia moyowangu natokwa hadi machozi.!!
************************************
NB:
Kila aliyejaaliwa uhai na afya njema ni wajibu (lazima) kufunga, kwani
ni amri kutoka kwa Allah Jalla Jalaal!! Usiache kufunga kwa makusudi tu! Ikiwa umefikwa na Maradhi basi Allah ndiye mjuzi zaidi. Anajua yaliyo
ya siri na ya dhaahiri, anajua yaliyofichikana ndani ya vifua vyetu na
Allah humlipa mja kutokana na nia!
•••••••••••••••••••••••••••••••••
SHAIRI : SITAFUNGA RAMADHANI!.
Reviewed by Abdurazak Ngowo
on
May 28, 2017
Rating:
No comments: